Mchakato wa Kuandaa Kitabu cha Chimbuko, Muundo na Historia ya Ukoo wa Kivenule na Uhehe kwa Ujumla

Mchakato wa Kuandaa Kitabu cha Chimbuko, Muundo na Historia ya Ukoo wa Kivenule na Uhehe kwa Ujumla
Karibu uone yale ambayo KAUKI inafanya

Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI, 2014

Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI, 2014
Chimbuko na Muundo wa Ukoo wa Kivenule (2005 - 2009)

Mkutano Mkuu wa10 wa KAUKI

Mkutano Mkuu wa10 wa KAUKI
Tangazo la Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI

Friday 15 February 2013

Kangamoko Mbinde Mbinde

 Mtindo wa kizazi kipya ambao kwa kiasi kikubwa umemong'onyoa maadili ya Watanzania. Sijui kama taifa tunaelekea wapi, lakini kama jamii tuna wajibu mkubwa wa kukemia tabia hizi ambazo zinaendana na utandawazi.

 

Katibu wa Bunge, Spika Makinda wapingana



KATIBU wa Bunge, Thomas Kashilillah amepingana hadharani na bosi wake Spika wa Bunge, Anne Makinda kuhusu kurushwa moja kwa moja matangazo ya Vipindi vya Bunge.

Jana katika mkutano na waandishi wa habari katika Ofisi za Bunge, Kashilillah alisema kuwa ofisi yake inakusudia kutoonyesha matangazo ya moja kwa moja ya vikao vya Bunge vinavyofanyika mjini Dodoma kutokana na baadhi ya wabunge kukiuka kanuni za kibunge kwa kuvunja maadili.

Hata hivyo, kauli ya Kashilillah inapingana na ile ya Makinda aliyoitoa mjini Dodoma, Februari 8 wakati wa kuahirisha kikao cha 10 cha Bunge aliposema: “Naipongeza TBC (Shirika la Utangazaji la Taifa) kwa kuonyesha moja kwa moja matangazo na yote yanayoendelea bungeni.

“Kutokana na vurugu zilizotokea, ninaiomba Serikali kuiongezea ruzuku TBC ili kupata mitambo ya kisasa waweze kuonyesha vizuri matangazo yake, safari hii matangazo yalikuwa yanakatika katika sana,” alisema Makinda.

Hata hivyo, kauli hiyo wakati wa kufunga Bunge ilikuwa ni ya pili kwa Makinda kwani baada ya kutokea vurugu zilizoongozwa na baadhi ya viongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Makinda aliisifu TBC kwa kuonyesha kila kilichotokea bungeni na kuweka msisitizo kuwa lazima TBC isaidiwe ili kila kinachotokea ndani ya Bunge kionekane kwa wananchi.

Akizungumza jana kwenye Ofisi za Bunge, Kashilillah alisema kuwa vikao vinavyofanyika sasa mara nyingi vinakiuka kanuni na maadili ya shughuli za Bunge, jambo ambalo limesababisha baadhi ya wabunge kuinuka na kutoa kauli mbalimbali wakati mijadala ikiendelea.

Kashilillah alisema, utaratibu unafanyika na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), ili kuangalia namna ambavyo wataweza kuonyesha shughuli za Bunge kwa vipande vipande vilivyorekodiwa kwa maeneo yanayofuata kanuni na maadili ili kuficha taswira mbaya itakayojitokeza kwa wananchi.

“Kuna ukiukwaji mkubwa wa kanuni na maadili ya vikao vya Bunge, na si kwamba wanaofanya hivyo hawafahamu, isipokuwa wanafanya makusudi au wanatafuta umaarufu kupitia vikao hivyo. Kutokana na hali hiyo, tumeamua kukaa na TCRA ili kuangalia namna ambavyo tunaweza kurusha vikao vilivyorekodiwa badala ya moja kwa moja,” alisema.

Simu za matusi na kashfa
Akizungumzia suala la Spika Makinda kutukanwa na kukashifiwa, Dk Kashililah alisema kuwa, kwa kushirikiana na vyombo mbalimbali ameshawafahamu wote waliofanya hivyo na taratibu za kuwakamata zinaandaliwa.

“Tumeshawabaini, tunafahamu wanakoishi na namba zao tayari zimeanza kushughulikiwa. Hasa wale wote waliotuma ujumbe wa matusi au kupiga simu,” alisema.

Kuvunjwa kwa kamati
Kuhusu kuvunjwa kwa baadhi ya Kamati za Bunge, alisema kuwa Spika wa Bunge anaweza kuzivunja kutokana na sababu mbalimbali ikiwamo utendaji wake au ushauri unaotoka kwa viongozi wa vyama vyenye uwakilishi bungeni.
Alisema kutokana na hali hiyo, waliangalia kamati ambazo zinafanya kazi kwa mwingiliano na kuhamishia shughuli zile kwenye kamati nyingine kama ilivyokuwa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) ambayo shughuli zake zimehamishiwa kwenye Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC).

Spika aongezewa ulinzi

SPIKA wa Bunge, Anne Makinda ameongezewa ulinzi pamoja na kubadilishiwa namba za gari analotumia kutokana na vitisho anavyovipata kutoka kwa wananchi ambao wamekuwa wakimtumia ujumbe wa simu.
Taarifa ambazo Mwananchi imezipata zinaeleza kuwa hatua hiyo imekuja baada ya viongozi wa Chadema kutoa namba za Spika na kuzigawa kwa wafuasi wake waliofika kwenye mkutano uliofanyika kwenye Viwanja vya Mwembe Yanga, jijini Dar es Salaam hivi karibuni ili wamtumie ujumbe mfupi wa simu.

Hivi karibuni gazeti hili liliripoti kuwa Spika Makinda amepokea ujumbe mfupi wa simu zaidi ya 400 na kupigiwa simu zinazofikia 200 za kumkashifu na vitisho.
Taarifa zilizopatikana jana zinaeleza kuwa Spika Makinda amekuwa akitumiwa ujumbe mfupi wa vitisho ambavyo inaonyesha kuwa wananchi wana hasira naye na ndiyo maana ameongezewa ulinzi.


Vyanzo vyetu vya habari vimeeleza kuwa gari la Spika Makinda limebadilishwa namba kwa kuondolewa herufi S ambayo humaanisha Spika na kuwekwa namba nyingine ambazo bado hazijajulikana.


“Watu wanaomtumia ‘meseji’ wana hasira, wanaweza kumdhuru na ndiyo maana ameongezewa ulinzi. Hata magari yake aliyokuwa akitumia yamebadilishwa na kupewa mengine tofauti,” kilieleza chanzo chetu cha habari.


Spika Makinda mwenyewe alipopigiwa simu ili kueleza kuhusu suala hilo la kuongezewa walinzi simu yake ilikuwa ikiita tu bila kupokelewa.


Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah naye simu yake ilikuwa ikiita tu bila kupokelewa.Tangu Chadema wagawe namba hiyo baada ya kumtuhumu Spika pamoja na msaidizi wake, Job Ndugai kuwa amekuwa akipindisha kanuni wakati wa kuliongoza Bunge.


Taarifa zilieleza kuwa wamekuwa wakisumbuliwa na kutumiwa ujumbe za vitisho.Wakati hayo yakitokea, tayari Ofisi ya Bunge imesema itawachukulia hatua kali wale wote waliotumia lugha chafu kwa ujumbe mfupi ama kupiga moja kwa moja kwa Spika na Naibu wake.


Katibu Mkuu wa Bunge, Dk Kashililah juzi alisema kuwa kutoa namba si tatizo, bali kuzitumia namba hizo kinyume na taratibu ndiyo haitakiwi, jambo ambalo linaweza kusababisha baadhi yao kuchukuliwa hatua za kisheria.


“Wote waliotoa lugha za matusi kwa Spika Makinda na Naibu Ndugai watachukuliwa hatua za kisheria. Tutawatafuta kwa njia zote, hii itasaidia kuwa fundisho kwa watu wenye tabia kama hizo ambao wanapewa namba kwa manufaa ya wananchi, lakini wanazitumia kinyume chake,” alionya Kashililah.


“Tutawasaka kwa kila hali, tutawabaini tu kwa kushirikiliana na idara mbalimbali ikiwemo Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na Polisi ili wachukuliwe hatua kali.”
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema, John Mnyika alipoulizwa jana kuhusu msimamo wa chama chake baada ya kutoa namba hizo kwa wananchi alisema; “Bunge halijatuuliza ila wakituuliza tutajibu.”

GHARAMA YA DHULUMA NI HOFU



Spika yapaswa utende haki kwa kuzingatia sheria na kanuni za Bunge

Katika hali ya kuwa na hofu kutokana na yaliyojitokeza katika Bunge la hivi karibuni, Spika wa Bunge, Anne Makinda ameongezewa ulinzi pamoja na kubadilishiwa namba za gari analotumia kutokana na vitisho anavyovipata kutoka kwa wananchi ambao wamekuwa wakimtumia ujumbe wa simu.


 


Ni vyema ndugu Makinda akajiuliza hii hofu ya kuongezewa ulinzi inatokana nini, kwa sababu hali haikuwa hivi siku za nyuma. Kuna msemo wa kidini ambao unasema kuwa, "Gharama ya Dhambi ni Mauti". Lazima ndugu Makinda atambue kuwa anachowafanyia Wabunge wa upinzani Bungeni, pia anawafanyia wananchi waliowatuma wabunge hao. 

 


Kwa hiyo, kama wawakilishi wa wananchi hawa maskini wanakwazwa na mtu mmoja au wawili kuwasilishwa kilio cha wananchi walio wengi kwa sababu zisizo za msingi, na atambue kuwa anatenda dhambi ya dhuluma. Na mara nyingi dhuluma ya wengi ni msiba na pia ni hatari sana.


 


Kitendo cha Wabunge wa Upinzani kuamua kutoa namba za simu za Spika na Naibu wake kwa wananchi, ilikuwa ni kuwashtaki na wategemee kupokea simu au ujumbe ambao hautakuwa na lugha njema kwao kwa sababu wamedhulumiwa sehemu ya haki zao.


 


Tatizo la elimu na maji si geni kwa Watanzania walio wengi maskini. Maji yamekuwa yakitoka sehemu ambako wakubwa na watu wenye hadhi na uwezo wanakoishi. Sehemu ambazo wanaishi walalahoi ambao Mhe. Mnyika alikuwa anawasemea, hamna maboma na pengine hayapo kabisa. Kwa kifupi, matatizo ya elimu na maji yanawagusa moja kwa moja wananchi wa kawaida.


 


Kuendelea kuporoka kwa kiwango cha elimu ni kikwazo kikubwa kwa watanzania walio wengi kwa sababu kunawanyima fursa watoto wao kuendelea mbele kielimu na kuishia mitaani na kuharibikiwa. Endapo mfumo wa elimu ungekuwa ni mzuri, wananchi walio wengi maisha yao yangekuwa yameboreka kwa sababu kuongezeka kwa fursa kwa watoto waliosomo.


 


Watoto wa hao viongozi ambao wanapinga hoja za msingi za matatizo yanayowakabili wananchi, wanasomo nje ya nchi au kwenye shule zenye hadhi ya juu hapa Tanzania. Wao wana uwezo wa kulipa mamilioni ya pesa ili watoto wao wafanikiwe kielimu. Lakini kwa mtoto wa Maskini hali ni tofauti kwa sababu yeye anaendelea kusota kwenye shule za Kayumba ambazo hazina walimu, vifaa wala tija kwa maisha ya sasa ya kidijitali.


 


Kwa hiyo, ulinzi wa Spika upo kwa wananchi wenyewe na siyo polisi. Ni vyema Mhe. Makinda akaondoa tofauti na upendeleo ambao amekuwa akiuelekeza kwa upande wa serikali na kurudi kwa wananchi. Natumaini mahusiano mazuri baina ya makundi haya mawili yatarudi na kuwa kama zamani. Kumbuka siku zote kuwa, "Mshahara wa Dhambi ni Mauti".

Wednesday 13 February 2013

GHARAMA YA DHULUMA YA HAKI YA WANANCHI



Katika Bunge lililoisha hivi karibuni, Wabunge wa Upinzani kwa pamoja waliungana kuupinga mpango wa Spika na Naibu wake wa kuendelea kuzizima hoja zao na pia kuongoza Kiti bila kufuata Kanuni kama wao Wabunge wanavyohimizwa kufanya hivyo.

Hii ilitokea kutokana na Hoja Binafsi ya Mhe. James Mbatia Kuzimwa. Hoja hiyo ya Mhe. Mbatia ilihusu suala la Mitaala, ikiiomba serikali kuiwasilisha Bunge ili iwe kujadiliwa kutokana na kuendelea kuporomoka kwa elimu hapa nchini.

Hoja Binafsi ya Pili kuzimwa ilikuwa ni Mbunge wa CHADEMA wa Jimbo la Ubungo, Mhe. John Mnyika, ambayo ilihusu hali ya huduma ya maji katika Jiji la Dar es Salaam, hasa akingalia wastani mdogo wa watu wanaopata maji safi na Salama. Hoja yake hiyo ilibainisha baadhi ya mapungufu ni kutotekelezwa kwa ahadi ya maji kama zilizovyoainishwa kwenye Ilala ya Uchaguzi ya CCM mwaka 2005 na mwaka 2005. Hali ya tatizo la maji linaonesha kuwa katika wastani wa watu 2 mtu mmoja hapati maji safi na salama.

Pamoja na Spika huyo kushindwa kutoa majibu ya rufani mbalimbali zilizoelekezwa kwake mwaka 2011 - 2012, ili kubaini kama anaongoza Bunge kwa mujibu wa sheria au anaongozwa kwa matakwa yake.

Katika Mkutano wa Wabunge wa CHADEMA waliokuwa Bunge uliofanyika Temeke mwisho Jijini Dar es Salaam, Wabunge hao waliamua kutoa namba ya simu ili itumike kumwambia Spika na Naibu Wake Wajiuzulu kwa kushindwa kuwajibika kikamilifu katika kulisimamia Bunge. 

Wananchi wameitikia wito huo na sasa na licha ya baadhi ya watu kuanza kuwatetea kutokana na kuwa na maslahi binafsi juu ya maamuzi ya viongozi hao. 

Hapa chini ni utetezi wao.


Wanachama wa CCM Mkoa wa Iringa, wamelaani vikali kitendo cha baadhi ya wafuasi wa Chadema kutuma ujumbe mfupi wa simu za mkononi kumkashifu Makinda huku baadhi yao wakipendekeza chama hicho kifutwe kwa kukosa ustaarabu.

Katibu wa Baraza la Wazee wa CCM Wilaya ya Iringa, Said Mdota alisema kitendo alichofanyiwa Spika Makinda si cha kiungwana na hakikubaliki na wapenda amani wote. Mdota alipendekeza wahusika wote wasakwe na wachukuliwe hatua kali za kisheria.

Naye Mwenyekiti wa Jumuiya wa Wanawake Mkoa wa Iringa, UWT, Zainab Mwamwindi alisema jumuiya hiyo inatarajia kukutana kesho pamoja na agenda nyingine itajadili suala hilo na kulitolea tamko.

 “Sisi kama wanawake na Spika ni mwanamke, suala hili limetudhalilisha sana na katika hili tunalikemea kwa nguvu zote na Februari 14, tunatarajia kufanya kikao cha Kamati ya Utendaji tutalijadili na kulitolea tamko,” alisema.

Monday 11 February 2013

REJEA YA MBUNGE MSIGWA MWAKA JANA NA YANAYOTOKEA LEO BUNGENI

Mheshimiwa Peter Msigwa (CHADEMA), Mbunge wa Iringa Mjini, mwaka jana Juni 2012 wakati wa Bunge la Bajeti, alikemea tabia mbaya ya wabunge na baadhi ya viongozi, kukwepesha ukweli kuhusu matatizo yanayowakabili wananchi na badala yake kuzungumzia masuala yasiyo na kichwa wala miguu. Maneno yake yanashahibiana na hali ilivyojitokeza katika bunge lililomaliza muda wake, Ijumaa iliyopita ya mwezi Februari 2013. 

Mheshimiwa Msigwa alizungumzia masuala mengi ya msingi ikiwemo ongezeko la Deni la Taifa hadi kunifikia trilioni 20. Kwa sasa deni la Taifa ni Trilioni 21. Deni linazidi kukua huku umaskani na uduni wa maisha ukiendelea kuongezeka. 

Mheshimiwa Mbunge alizungumzia pia suala la kujitathmini na kujihoji kama kweli tunawajibika ipasavyo hasa ikizingatiwa kuwa kuna ongezeko la utegemezi hasa watoto, ambao kwa kiwango kikubwa inabidi kulishwa na kusomeshwa na taifa hili.

Ifuatayo ni hotuba yake kwa kifupi....
   

Tuesday 5 February 2013

BUNGE LAAHIRISHWA TENA LEO BAADA YA KUTOLEWA KWA HOJA KALI TOKA UPANDE WA UPINZANI




BUNGE LAAHIRISHWA TENA LEO BAADA YA HOJA NZITO kutolewa na Wabunge wa Upinzani ikiwemo suala la Spika kutokuzingatia Kanuni za bunge katika utendaji wa kazi zake.

Spika Anna Makinda pia leo amekataa hoja ya Nasari kwa sababu zisizo la lazima, eti shughuli za siku zinapangwa na Kamati ya Uongozi. Kwa hiyo hoja hiyo haitaweza kujadiliwa.

Mhe. Lissu pia amekumbushia baadhi ya rufaa dhidi ya maamuzi ya Spika ya 2011 - 2012 yaliyofanyika nje ya kanuni, lakini mpaka leo hazina majibu. Spika pia akajitetea kuwa, kwa masuala yaliyotokea siku ya Jumatatu, hakuna rufaa yeyote iliyokatwa.

Licha ya Mbunge wa Ubungo kuonenesha wasiwasi wake kwa Waziri wa Maji kuvunja kanuni ya 57c ya Kanuni za Bunge kwa kuzungumza vitu ambavyo ambaviandika na kuvipanga mwenyewe. Spika alitoa majibu ya kuwa Waziri hakuvunja kanuni.

Hivi ndivyo bunge linavyoendeshwa bila ya kuzingatia kanuni.

HALI ILIVYOKUWA BUNGENI DODOMA JANA

Kweli Naibu Spika ameshindwa kabisa kulimudu Bunge letu. Angalia video hii

 


Bunge lachafuka

*Wabunge wapiga kelele, wamzomea Naibu Spika
*Bunge lalazimika kuahirishwa kabla ya wakati


NAIBU Spika wa Bunge, Job Ndugai, jana alilazimika kuahirisha Bunge kabla ya wakati. Tukio hilo la aina yake, lilitokea jioni, baada ya kutokea hali ya kutoelewana kati ya wabunge wa upinzani na wapande wa CCM.

Dalili za Bunge kuvunjika zilianza mapema, baada ya wabunge kuingia bungeni katika kipindi cha jioni wakati Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe, alipowasilisha hoja yake kwa dakika 25 badala ya 15 zinazoruhusiwa kwa mujibu wa Kanuni za Bunge.

Kutokana na Profesa Maghembe kutumia muda mwingi unaodaiwa kwenda kinyume cha kanuni za Bunge, Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (CHADEMA) alisimama na kuomba Mwongozo wa Spika, akionyesha kutoridhishwa na muda aliotumia Profesa Maghembe.

Katika maelezo yake, mbunge huyo alisema Profesa Maghembe alitakiwa kutumia dakika 15 na siyo zaidi ya hapo.

Baada ya Lissu kujenga hoja hiyo, Naibu Spika, alikiri Profesa Maghembe kutumia muda mwingi, lakini akajitetea kwamba kosa hilo limesababishwa na makatibu wa Bunge na kwamba waliteleza katika hilo.

Pamoja na kukiri kosa hilo, alimruhusu Profesa Maghembe aendelee kuwasilisha hoja yake kwa dakika tatu zaidi ili amalizie alichokuwa akikiwasilisha.

Baada ya Naibu Spika kusema hayo, wabunge wa upinzani waliokuwa wakiongozwa na Lissu, ambaye pia ni Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani Bungeni, walisimama na kuanza kuzomea wakionyesha kutoridhishwa na uamuzi wa Naibu Spika.

Hali ilipokuwa hivyo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, alisimama kutoa mwongozo, lakini hakusikilizwa, kwa kuwa wakati huo Bunge lilikuwa limetawaliwa na kelele. Kutokana na hali hiyo, aliamua kukaa kwa kuwa hakukuwa na hali ya utulivu.

Wakati wabunge wakipiga kelele, Naibu Spika alikuwa amekaa kimya kwa muda wa dakika zipatazo mbili, kisha akasimama na kuahirisha Bunge.

Hata hivyo, wakati kelele hazijazidi bungeni, Naibu Spika kabla hajaahirisha Bunge, alisikika akiwataka wabunge wanaotaka kujadili hoja ya Waziri wajiorodheshe.

Baada ya Bunge kuahirishwa, Naibu Spika pamoja na Lissu alikutana nje ya Ukumbi wa Bunge na kuanza kunyoosheana vidole, wakitoleana maneno yasiyofaa.

Naibu Spika azungumza
Naibu Spika, Job Ndugai, alipozungumza na waandishi wa habari nje ya Ukumbi wa Bunge, alitetea uamuzi wa kumzidishia muda Profesa Maghembe, kwa kuwa hoja yake ndiyo iliyokuwa ikitakiwa kujadiliwa.

Jaji Werema anena
Naye Jaji Werema aliwaambia waandishi wa habari, kwamba kilichotokea bungeni siyo jambo la ajabu kwa mabunge yenye mfumo wa vyama vingi.

“Alichofanya Naibu Spika kilikuwa sahihi kwa sababu kanuni zinasema kama kuna hoja mbili zinazohitaji kujadiliwa, ile ya Serikali ndiyo inapewa umuhimu wa kwanza.

“Kanuni ziko wazi, kwamba Mbunge yeyote anaweza kusimama na kutoa hoja, lakini ile ya Serikali lazima ipewe kipaumbele kwanza, lakini hilo halikukubaliwa ndiyo maana ya songombingo mliyoona pale.

“Katika hili, hatuwezi kukwepa, kwani hii siyo mara ya kwanza jambo kama hili kutokea. Mimi nilisimama ili nitoe angalizo, kwamba hoja zote mbili, ile ya Mnyika na ya Waziri Maghembe, zote zinaweza kujadiliwa kwa pamoja, lakini hawakukubali, waliendelea na vurugu.

Mnyika anasemaje?
Kwa upande wake, Mbunge wa Ubungo, John Mnyika, aliwaambia waandishi wa habari, kwamba, hoja yake ilikataliwa na Naibu Spika tangu awali.

“Utaratibu haukufuatwa tangu mwanzo, mliona nilikatazwa kuingiza marekebisho ya hoja zangu, ingawa walizipokea tangu jana na lengo lao lilikuwa kuzuia hoja iondolewe,” alisema Mnyika.

Awali Mnyika aliwasilisha hoja binafsi akitaka upatikanaji wa maji uwe sehemu ya hitaji muhimu la binadamu.

Kwa mujibu wa Mnyika, kama maji salama yakipatikana, umasikini utapungua kwa kuwa ukosefu wa maji salama nsiyo unaochangia umasikini huo.

Kuhusu Jiji la Dar es Salaam, alisema hadi kufikia mwaka 2011, lilikuwa likikadiriwa kuwa na watu wapatao milioni nne hadi tano, lakini halina maji ya uhakika.

Akijenga hoja yake, alisema upatikanaji huo wa maji baada ya uhuru mwaka 1968 ulikuwa asilimia 68, lakini miaka 50 baadaye upatikanaji huo umekuwa asilimia 55 tu tena ya mgawo.

Kutokana na hali hiyo, aliitaka Serikali ishughulikie mpango wa dharura wa kupunguza kero ya maji uliowekwa na Wizara ya Maji, kwa kushirikiana na DAWASA tangu Juni 2010.

Pamoja na hayo, aliahidi kukata rufaa dhidi ya kiti cha Spika, baada kuzuiwa kuingiza maneno mengine katika hoja yake aliyokuwa akiiwasilisha.




NDUGHAI BUNGE LIMEKUSHINDA



WABUNGE wa upinzani jana walizua tafrani bungeni na kusababisha kikao kilichokuwa kikiongozwa na Naibu Spika, Job Ndugai kuvunjika kabla ya muda uliokuwa umepangwa.
Wabunge hao wa upinzani walisimama wote kwa pamoja na kuanza kupiga kelele za kupinga hatua ya Ndugai kuruhusu kujadiliwa kwa hoja ya Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe.
Profesa Maghembe katika hoja yake ambayo iliungwa mkono na wabunge wa CCM, alikuwa akipendekeza kuondolewa bungeni kwa hoja binafsi iliyokuwa imewasilishwa mapema na Mbunge Ubungo (Chadema), John Mnyika.

Mnyika katika hoja yake alikuwa akitaka Bunge liazimie kuitaka Serikali ichukue hatua za haraka ya kuboresha upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa majitaka katika Jiji la Dar es Salaam.

Baada ya Ndugai kuruhusu hoja ya Profesa Maghembe kujadiliwa badala ya hoja ya Mnyika, wabunge wa upinzani walisimama na kuanza kupiga kelele za kupinga kile walichodai kwamba ni Naibu Spika kuvunja kanuni ambazo anapaswa kuzisimamia.

Ilivyokuwa
Profesa Maghembe aliyekuwa mchangiaji wa kwa nza katika hoja ya Mnyika alitoa kauli kwamba Serikali inaendelea kukamilisha miradi mbalimbali ya maji jijini Dar es Salaam, hivyo kutaka hoja ya Mnyika iondolewe.

Kabla ya kutamka maneno hayo, tayari wabunge wa upinzani bila kujali vyama vyao walikuwa wameanza kumzomea na kupiga kelele kiasi kwamba maneno yake ya mwisho hayakusikika.

Baada ya hapo alisimama Naibu Spika na kuwataka wabunge watulie ili waanze kuchangia hoja hiyo na alimtaka Mnyika kuzungumza, lakini kabla ya Mnyika, Mbunge wa Kawe, Halima Mdee alisimama na kuanza kuzungumza baada ya Naibu Spika kumruhusu.

“Mheshimiwa Naibu Spika naona mwendelezo wa uvunjwaji wa taratibu na kanuni za Bunge, hoja binafsi zinaratibiwa na kanuni ya 57 na 58,”alisema Mdee na kuongeza;
“Kanuni hizi mbili ukizisoma sioni Waziri anatakiwa kueleza kipengele gani kitoke…….”

Kabla Mdee hajamaliza kueleza Naibu Spika, alisimama na kumtaka Mnyika achangie kama alikuwa ana la kusema, lakini akamkatisha na kelele zikaanza bungeni.
Mnadhimu wa Kambi ya Upinzani, Tundu Lissu alisimama kutaka utaratibu, lakini Naibu Spika Ndugai alimkatisha kisha akasema “Waswahili wanasema kuchamba kwingi……”

“Wewe ni “Chief Whip” (Mnadhimu Mkuu) upande wa Serikali umetoa hoja na sisi tunachangia hivyo tunachangia sasa,” alisema Naibu Spika na kumwita Mdee aendelee kuchangia.

Hata hivyo, Mdee alikataa na Naibu Spika alimwita Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Zarina Madabida kuendelea kuchangia.

“Mheshimiwa Naibu Spika nakushukuru kwa kunipa nafasi na naipongeza Serikali kwa kazi nzuri inayoifanya,” alisema Madabida, lakini kabla hajaendelea baadhi ya wabunge wa upinzani walianza kutaka kutoa taarifa na kusimama wakati Naibu Spika naye amesimama hivyo Bunge kukwama kuendelea kwa muda.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick We rema alisimama na wakati alipoanza kuzungumza wabunge wote wa upinzani walianza kuimba CCM, CCM, CCM huku wakigonga meza.

Kitendo hicho kilisababisha Jaji Werema kwenda kwenye meza ya Spika ili azungumze na Naibu Spika, lakini kelele ziliendelea na Ndugai akasema, “Siahirishi Bunge ili Watanzania wajue nani anavuruga na wajue pia mbivu na mbichi.”

Aliwataka wabunge waliokuwa wakiimba na kupiga kelele kuendelea huku shughuli za Bunge zikiwa zimesimama kwa muda. Baada ya mazungumzo mafupi kati ya Werema na Ndugai, Naibu Spika alisimama na kuhoji wangapi wanaunga mkono hoja ya Serikali na wangapi wanaikataa hoja ya Mnyika kitendo ambacho hakikueleweka, lakini Ndugai akasema hoja imeondolewa.

“Naliahirisha Bunge nataka Kamati ya Uongozi ya Bunge kukutana,”alisema Ndugai huku wabunge wa upinzani wakiwa wanapiga kelele. Hata hivyo, Werema alisema kuwa Bunge litamwajibisha, Lissu kwa kutoa lugha ya matusi bungeni.

Mvutano asubuhi
Wakati hayo yakitokea katika katika kikao cha jana asubuhi mvutano mkubwa uliibuka pale baadhi ya wabunge walipokuwa wakilumbana kiasi cha kutoleana maneno ya kashfa, kinyume cha Kanuni za Bunge.

Malumbano hayo yaliwahusisha Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu dhidi ya Mbunge wa Nzega (CCM), Dk Hamis Kigwangalla, mvutano ulitokana na mjadala wa hoja binafsi ya Kigwangalla.

Katika hoja yake mbunge huyo alilitaka Bunge kupitisha azimio la kuitaka Serikali ianzishe mpango maalumu wa kukuza ajira kwa vijana kwa kuanzisha mfuko wa mikopo ya vijana wanaowekeza kwenye kilimo na viwanda vyenye uhusiano wa moja kwa moja na kilimo.
Katika mchango wake, Lissu aliishambulia hoja hiyo kwa kusema kuwa haikuwa na msingi wa kuwasaidia vijana na badala yake ilikuwa ni hoja ya ‘kutongozea kura za mwaka 2015’.

Jana Lissu pia alitoa taarifa kwamba hoja hiyo ya Dk Kikwangalla haikuwa na ubunifu kwani wakati akipendekeza kuundwa kwa mfuko wa mikopo, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Dk Fenella Mukangara alisema mfuko wa vijana umekuwapo tangu 1994. Kutokana na kauli hizo, Kigwangalla alipokuwa akihitimisha hoja yake, alimshambulia Lissu kwa kusema:

“Tundu Lissu ni mnafiki, kazi yake ni kupinga kila kitu kinacholetwa mbele yake hata kama ni kizuri yeye anafanya kazi ya kupinga, lakini nasema kuwa ana matatizo na mimi kama daktari wake nayajua.”

Vuta nivute hiyo, ilisababisha wabunge John Mnyika, Moses Machali, Felix Mkosamali, Ester Bulaya na David Silinde kusimama na kupiga kelele za kuomba mwongozo wa Spika.

Hata hivyo, mbunge huyo aliwashambulia wabunge hao kwa kusema “Mheshimiwa Naibu Spika, tulishaambiwa hapa na Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kuwa wanaume wanapozungumza lazima vijana wanyamaze, naomba wabunge wote waliosimama wakae chini niwape dozi.”