Mchakato wa Kuandaa Kitabu cha Chimbuko, Muundo na Historia ya Ukoo wa Kivenule na Uhehe kwa Ujumla

Mchakato wa Kuandaa Kitabu cha Chimbuko, Muundo na Historia ya Ukoo wa Kivenule na Uhehe kwa Ujumla
Karibu uone yale ambayo KAUKI inafanya

Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI, 2014

Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI, 2014
Chimbuko na Muundo wa Ukoo wa Kivenule (2005 - 2009)

Mkutano Mkuu wa10 wa KAUKI

Mkutano Mkuu wa10 wa KAUKI
Tangazo la Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI

Wednesday 9 January 2013

CHIMBUKO NA HISTORIA YA UHEHE

TAARIFA YA UJUMLA YA CHIMBUKO NA HISTORIA YA UHEHE

Historia ya Wahehe ni pana sana na ina machimbuko tofauti kwa mujibu wa taarifa mbalimbali za kitafiti ambazo tayari zimekwishafanyika. Koo nyingi za Kihehe zipo kutokana na tabia tofauti za kimaisha zilizojumuisha shughuli mbalimbali za kijamii mfano ufugaji, uwindaji, ufuaji chuma, uwezo wa vita na kilimo. Jamii za Koo zilizojishughulisha katika shughuli za namna hii ziliweza kutambulika kirahisi na jamii nyingine. 

Kuna asili (chimbuko) mbalimbali za Kabila la Wahehe. Kuna Wahehe wenye asili ya Uhabeshi, Wahehe wenye asili ya Ungazija na pia Wahehe wenye asili ya Wanitole. Kuna taarifa fupi kuhusiana na baadhi ya asili hii, lakini ninaweza kusema kidogo kwa Wahehe wenye asili ya Wangazija huko mbeleni. 

Hata majina ya Koo hii yalibeba maana nzima ya historia na aina ya shughuli zinazofanywa na jamii hizo. Kwa mfano Koo za akina Chusi zilikuwa na umaarufu katika shughuli za ufuaji chuma na utengenezaji wa zana zinatokanazo na chuma. Mpaka leo hii, asili ya koo za akina Chusi ni wafuaji na wahunzi wa zana zinazotokana na chuma. 

Kuna majina katika koo fulani yalipatikana kutokana na mfululizo wa majanga mbalimbali ya asili mfano vifo. Koo ambazo zilikuwa na bahati mbaya ya kupoteza watoto mara tu wazaliapo ziliweza kujulikana kwa majina fulani kwa wachache ambao waliweza kuepukana na majanga hayo. Kwa mfano Koo za akina Mponela, zinatokana na maana halisi ya neno Kupona kwa kiswahili. Hii ni jamii ya watu wachache ambao waliweza kupona kutoka kwenye janga la vifo.

 

Koo nyingine zilikuwa ni maarufu katika upiganaji wa vita katika maeneo mbalimbali ndani ya Himaya ya Uhehe na nje ya Himaya Uhehe. Kutokana na umahiri wao katika vita, Koo hizi ziliongozwa na Machifu au Watemi kwa lugha ya Kihehe. Baadhi ya Koo hii ni pamoja na akina Mduda, Kivenule, Mkwavinjika, Mnyigumba, Myinga na Lumaco. 

Majina ya Koo hizi ambazo zilijihusisha katika vita mengi yao ni ya sifa kutokana na umahiri wao katika vita. Yawezekana ni katika shabaha, kutumia zana za kivita na pia imani ambayo ilikuwa ni msingi wa mfanikio yao katika vita. Kwa mfano matumizi ya madawa ya asili ambayo yaliongeza hamasa na chachu ya ushiriki katika mapigano vitani. Kwa mfano Ukoo wa KIVENULE, unatokana na neno KUVENULA. 

Historia ya Ukoo wa Kivenule inaletwa na mtu mmoja aliyeitwa Tagumtwa Mtengelingoma Balama. Mzee Tagumtwa Balama (KIVENULE) ndiye aliyewazaa Mzee Tavimyenda Kivenule na Mzee Kalasi Kivenule. Ikumbukwe kuwa, jina halisi la ukoo wa Kivenule ni BALAMA. Neno KIVENULE linamaanisha sifa ya kuwa jasiri Vitani na hasa katika kutumia silaha za asili za Mishale na Mikuki yaani kwa Lugha Asilia ya Kihehe “MIGOHA” katika kupambana na adui katika vita za kikabila enzi hizo.  Kwa maana hiyo, kwa Kihehe LIGALU ni Vita. Vatavangu walikuwa ni wakuu wa Vita au wapiganaji vitani. Kuhoma maana yake Kumchoma adui kwa sila ya jadi mfano Mkuki, Upinde au Mshale. Migoha maana yake Mikuki. Venula maana yake ua, fyeka maadui. 

LIGALU ndiyo iliyochangia kuzaliwa kwa jina la Ukoo la KIVENULE. KIVENULE maana yake ni Ushujaa kutokana na Shabaha ya Mikuki. 

KUVENULA lilibeba maana halisi ya uwezo wa kuwa na shabaha ya kuwaangamiza maadui kwa kutumia silaha ya Mishale na Mikuki. Babu yetu TAGUMTWA BALAMA alilidhihirisha hili katika Vita na Watavangu na hivyo kusababisha kuzawadiwa kwa jina la KIVENULE kama jina la sifa kutokana na ushujaa katika Vita. 

Baada ya kuwazaa watoto hawa wawili yaani TAVIMYENDA na KALASI, walisafiri na kufika hadi sehemu ya KALENGA, wakiwa katika harakati za kutafuta maisha. Ndipo Babu TAVIMYENDA KIVENULE alipoombwa na Mzee MYINGA aende akamsaidie kumchungia mifugo yake eneo la MAGUBIKE na pia Babu KALASI KIVENULE naye kuamua kwenda eneo la ILOLE kutafuta maisha. 

Akiwa eneo la MAGUBIKE, Babu Tavimyenda Kivenule akafanikiwa kupata watoto Saba (7), yaani BABU KAVILIMEMBE KIVENULE, BABU MGAYAFAIDA KIVENULE, BABU SIGATAMBULE KIVENULE, BIBI MGASI KIVENULE, BIBI MALIBORA KIVENULE, BIBI SIGINGULIMEMBE KIVENULE, BABU ABDALAH KIVENULE NA BIBI SIKIMBILAVI SEMABIKI.  Huyu Bibi Sikimbilavi Semabiki hakuwa mtoto wa Babu Tavimyenda ila alikuwa ni mtoto wa kufikia kwa  Bibi yetu.

Baadhi ya akina Babu walifanikiwa kuwa na wake zaidi ya mmoja na hawa walikuwa ni Babu SIGATAMBULE KIVENULE, ambaye mke wake wa kwanza alikuwa anaitwa SIWANGUMHAVI SINGAILE, mke wake wa pili alikuwa anaitwa  NYANYILIMALE SINGAILE na mke wa Tatu, PANGULIMALE SETWANGA. Mke wa pili na tatu wa Babu Sigatambule bado wapo hai. 

Babu HUSEIN KIVENULE naye alikuwa na wake wawili ambao ni YIMILENGERESA SEMSISI na DALIKA SETALA. Taarifa za wake wa Babu wengine bado zinaendelea kufanyiwa utafiti. Babu MGAYAFAIDA KIVENULE yeye hakubahatika kuoa wala kuwa na mtoto. Alikuwa ni mlemavu na ndiyo maana ya jina lake MGAYAFAIDA. 

Kwa upande wa ILOLE, Babu KALASI KIVENULE alibahatika kuwa na watoto watatu ambao ni Babu SALAMALENGA (KAHENGULA) KIVENULE, MGUBIKILA (NYAKUNGA) KIVENULE NA SEKINYAGA KIVENULE. 

BABU SALAMALENGA KIVENULE alikuwa mwanaume peke yake na wawili waliobaki walikuwa ni wanawake. Babu Salamalenga Kivenule alioa wake watatu ambao ni Bibi NYANGALI, BIBI SEMFILINGE MHENGAATOSA NA BIBI SEMKONDA CHOGAVANU. Kupitia kwa wake zake watu, Babu Salamalenga ndiye aliyeeneza Ukoo wa Kivenule katika maeneo ya Nduli, Ilole, Mgongo na Kigonzile. 

MABORESHO YA TAARIFA ZILIZOPO KUHUSU HISTORIA YA UKOO WA KIVENULE

Kwa mujibu wa taarifa za kihistoria kutoka eneo la ILOLE inaonesha kuwa, Babu Salamalenga alitokea Magubike na kuelekea eneo la Kaskazini. Baadaye kulitokea ugomvi baina ya makabila, na hivyo kusababisha vita. Salamalenga akapelekwa eneo la Pawaga Vitani, ambako alipigana mpaka vita ilipoisha. Baada ya kurudi toka Vitani, Babu Salamalenga alifanikiwa kupata wake watatu, yaani Bibi Nyangali, Bibi Semfilinge na Bibi Semkonda. Hawa wake zake wote wa watatu alifanikiwa kuzaa nao watoto. 

Awali, Bibi Semkonda aliolewa na Mwamatagi na kuzaa mtoto analiyeitwa Sipanganakumutwa Sematagi. Semnyawanu wapo Kalenga na ni watoto wa Sipanganakumtwa. 

Watoto wa kila mke wake wameooneshwa kama ifuatavyo:
1.    Bibi   Semkonda
  • Pangayena           Kivenule
  • Jonas                  Kivenule
  • Samwel               Kivenule
  • Balasamaneno      Kivenule
  • Daud (William)     Kivenule
  • Barton                 Kivenule
2.    Bibi Semfilinge

  • Chogavanu          Kivenule
  • Munguatosa         Kivenule
  • Mwilimilisa (Gungamesa) mtoto wa Sekinyaga
3.    Bibi Nyangali

  • Tindasulanga        Kivenule
  • Sigondola             Kivenule
  • Shaban                Kivenule
  • Gungamesa          Kivenule

Mpaka, inaonyesha katika historia ya Ukoo wa Kivenule kuwa Babu Kalasi alimzaa Babu Salamalenga.  

Katika Mkutano Mkuu wa Tatu wa KAUKI, wawezeshaji wa Mada ya Chimbuko na Historia ya Ukoo, bado hakujawa na taarifa rasmi zinazojitosheleza kuhusiana na mtiririko wa kizazi hiki cha Ukoo wa Kivenule. Katika mkutano wa Tatu wa KAUKI, wawezeshaji walibainisha kuwa, muundo wa Ukoo kwa upande wa Kidamali na Magubike upo kama ifuatavyo:

Babu Mtengelingoma Balama alimzaa Babu Tagumtwa. Pia, Babu Tagumtwa alikuwa na wake wawili (2); yaani Bibi Sesambagi na mwingine ambaye jina lake halikuweza kuandikwa (patikana) ambaye alimzaa Babu Kalasi. 

Babu Tavimyenda ambaye ni mtoto wa Babu Mtelingoma, alikuwa na wake watatu (3) ambapo mmoja wa wake zake alikuwa anaitwa Bibi Mkami Sekabogo. Bibi Mkami Sekabogo alikuwa na mtoto wake wa kwanza ambaye aliitwa Sikimbilavi Semabiki.  Mtoto huyu alimzaa kwa mme mwingine. Baadaye alipokuja kuolewa na Babu Tavimyenda, aliweza kuwazaa watoto wafuatao:
  1. Myumbila       (Kavilimembe) Kivenule
  2. Mgaifaida       Kivenule
  3. Sigatambule   (Matesagasi) Kivenule
  4. Hussein          Kivenule

Mke wa pili wa Babu Tavimyenda Kivenule aliwazaa watoto wafuatao:
  • Abdalah               Kivenule
  • Sigungilimembe    Kivenule
  • Malibora              Kivenule

Mke wa Tatu wa Babu Tavimyenda Kivenule alimzaa mtoto mmoja tu aliyejulikana kwa jina la Mgasiyumhavi Kivenule. 

Nao watoto wa Babu Tavimyenda kwa Mke wake Bibi Mkami Sekabogo walijaliwa kuwa na familia zao isipokuwa kwa Babu Mgaifaida ambaye hakubahatika kupata familia. Babu Mgaifaida pia alikuwa mlemavu. 

Babu Kavilimembe ambaye pia ni mtoto wa kwanza wa Babu Tavimyenda Kivenule, alijaliwa kuwa na wake wawili na kuzaa nao watoto. Mke wa kwanza wa Babu Kavilimembe alikuwa anaitwa Bibi Sekusiga ambaye alizaa watoto wafuatao:

  1. Elizabert         Kivenule
  2. Dalikimale       Kivenule
  3. Sandra            Kivenule
  4. Pangalasi        Kivenule 

Mke Mdogo wa Babu Kavilimembe Kivenule ambaye pia alijulikana kwa jina la Sekusiga Mdogo alizaa watoto wafuatao:
  1. Salikuvaganga          Kivenule; na
      1. Francis            Kivenule

 WAHEHE WENYE ASILI YA UNGAZIJA

UNGAZIJA WA WAHEHE AU WANYALUKOLO

Kuna Wahehe wenye mchanganyiko wa Kihabeshi na pia Kingazija. Katika eneo hili, tutangalia zaidi, mchanganyiko wa Wahehe na kizazi cha Kingazija.
 

Pengine tungeangalia baadhi ya makundi ya Kihabeshi ambayo yanachangia katika kuliunda Kabila la Wahehe. Baadhi ya makundi ya WanitoleWahabeshi’ ya Wahehe, ni pamoja na VAHAFIWA walioishi sehemu za KALENGA, KIPAGALA, KIHESA, TAMBALANGOMBE, IBANANGOSI, TIPINGI, IKOLOFYA, NYAMBILA, KIBEBE, WELU na ISANZALA. Mtawala wao alikuwa MWALYELU aliyetawala WELU hadi PAWAGA ‘MAVAGA’ na MWAMWANO MWANSIGE aliyetawala WUTINDE. 

Majina ya watu wa kundi hili yalitokana hasa na KUFA kwao kwa wingi kwa njaa na maafa, hawa ni kina MWAMUGOVANO, MWAMALIGA, MWAMUKEMANGWA na MWAMUHESA. Husalimiana ‘kamwene HAFIWA’ au ‘KAMWENE MUPONELA’ ila kina MWACHAULA husalimiana ‘KAMWENE LUGOME’. VANYATENGETA ni kundi lililoshi maeneo ya UZUNGWA, KITELEVASI na LUNDAMATWE. 

Hawa walikuwa ni mafundi wa KUFUA CHUMA, walioishi kwenye milima yenye asili ya milipuko ili kutafuta mchanga wenye chuma, baadhi yao ni kina MWACHUSI na MWAMUVANGE. Salamu yao ni ‘KAMWENE TEGETA’ ila kina KALINGA husalimiana ‘KAMWENE HIGO’, wao hawali MBAWALA. 

VANYAKILWA ni watu walitokea KILWA na kuishi maeneo ya MUFINDI, hawa ni kina MWALWAGI na MWAKIHWELE, salamu yao ni ‘KAMWENE KILWA’. VASAVILA waliishi juu ya milima ya WELU SEHEMU ZA MAKUNGU, MAGUBIKE NA MATOGALU, hawa ni kina MWAMFILINGE na MWAKASIKE. VADONGWE ni kundi lililoishi pembezoni mwa vilima katika maeneo ya UHAMBINGETO, IPOGOLO, NYABULA na LUHOTA.

 

Wao ni mchanganyiko wa WANITOLE na WASUNGWA na salamu yao ni ‘KAMWENE HUVI’. Baadhi yao ni kina MWAMUYOVELA, MWAMALUVANGA na MWAMUKAKILWA. Makundi haya ya WAHEHE yanadhihirisha kuwa, wao ni mchanganyiko wa vizazi vya watu wa jamii tofauti tofauti. 

DAMU YA KINGAZIJA ILIVYOINGIA UHEHE NA KULETA UTAWALA WA MUYINGA, KIZAZI CHA MKWAVINYIKA (MKWAWA) 

Wenyeji wa asili wa IRINGA kabla ya MWAMUYINGA kuingia na kuanza kutawala, ni WASUNGWA, ukiwaacha WANITOLE kwa mujibu wa historia halisi iliyovurugwa na tawala za vikundi vya hao WANITOLE. 

WASUNGWA huishi katika safu ya milima ya USUNGWA iliyopo mashariki ya mji wa IRINGA. MWAMUYINGA ambaye pia ana majina ya MBUNSUNGULU, MWAKILYEMIKONGI, MUHUMBA, MDAGALUHANDO na LWIMATO, yaliyotokana na taabu alizozipata kutoka UKAGURU hadi MAHENGE, lakini jina lake halisi ni Hasani Yusufu, mjukuu wa Hasani Hasani, mtu aliyetokea UNGAZIJA kupitia USHELISHELI hadi pwani ya Afrika ya Mashariki, akitafuta VIPUSA, PEMBE za NDOVU na kufanya BIASHARA YA UTUMWA kama ilivyokuwa kawaida ya WAARABU wengi wakati huo. 

Alifika Kilwa Kisiwani na kushinda vita alivyopigana na kulowea huko kwa kuoa mwanamke wa Kiafrika aliyemzalia mtoto aitwaye Yusufu Hasani, aliyerithi usultani wake hapo baadaye na kumuoa mwanamke wa Kiafrika pia aliyekuwa binti Mulimba na kuzaa nae watoto wawili wa kiume, Hasani au ‘Mbunsungulu’ na Ahmad. 

Yusuf Hasani aliondolewa mamlakani na kuuawa na Wareno waliokuwa wanapiga vita utumwa. Hasani ‘Mbunsungulu’ na nduguye Ahmad walikimbilia Mafia walikopendwa sana na wenyeji wa huko na walianza kutawala huko, ambako Mbunsungulu alioa.

Wakati mkewe akisubiri kujifungua, taarifa za Wareno kutaka kuwafuata na kuwaangamiza baada ya kugundua kuwa wako huko, ziliwafikia kupitia kwa mjomba wao, Malik Sud, aliyenusurika kwenye mapambano Kilwa Kisiwani. Kwa hiyo, iliwalazimu Mbunsungulu, Ahmad na mjomba wao kukimbilia Ukaguru karibu na Kilosa.

Kabla ya kuondoka, Mbunsungulu alimuusia mkewe kuwa mtoto akizaliwa aitwe Wakinakuonewa. Mbunsungulu alioa tena huko alikokimbilia na mkewe alimzalia watoto watatu, Ngulusavangi, Mufwimi na Ngwila. 

Mama huyo alihama na kukimbia na watoto wake kutoka Ukaguru kuelekea Upogoroni, maeneo ya Ulanga huko Mahenge, baada ya Mbunsungulu, Ahmad na mjomba wao, kuvamiwa na Waarabu na kuuawa. 

Vijana hao watatu wakaondokea kuwa wawindaji hodari sana huko walikokimbilia na walikuwa hawanywi maji ya mito, kila jioni walichimba visima. Ugomvi uliowatenganisha ulitokana na jambo hilo pamoja na kitendo cha NGWILA kutangulia kuoa kabla ya kaka zake NGULUSAVANGI na MUFWIMI bila ya idhini yao. 

Kuna habari nyingi za vijana hawa wote watatu, lakini tutajihusisha zaidi na MUFWIMI ambaye uzao wake ndio ulimleta MUYINGA. 

MUFWIMI aliendelea na uwindaji akiwa na wafuasi wake MWILAPWA, MAFUMIKO na MABIKI pamoja na mbwa wawili; LUDOVIKO na MUHEPAPAKWIMA. 

Alisafiri hadi DABAGA katika maeneo ya NG’ULUHE akifikia kwanza IKOMBAGULU alikowaacha wafuasi wake kwa muda na kuendelea mbele kuwinda katika eneo lililotawaliwa na MWAMUDUDA. Huyu bwana alikuwa na uwezo wa kuua nyati hata kumi kwa siku, aliichoma nyama porini na kuipaka chumvi na kumtumia mtawala Mwamududa na kwa kuwa watu wa huko hawakuwa wanaijua chumvi bado, MWAMUDUDA alipoipata nyama hiyo iliyotiwa chumvi aliiona tamu sana. 

Chumvi ilimfanya Mufwimi apendwe na kupewa ruhusa ya kuwinda atakavyo na alipokaribishwa, aliomba mahala pa kulala akapewa nafasi nyumbani kwa mtawala MWAMUDUDA. Huko alianza kufanya mapenzi ya siri na binti wa MWAMUDUDA aliyekataa kuolewa na wanaume wengi waliojitokeza kumposa, hatimaye alimpa mimba. Alipoambiwa juu ya mimba hiyo na yule binti, aliagiza mtoto akizaliwa salama akiwa wa kiume aitwe MWAMUYINGA na akiwa wa kike aitwe SEMUYINGA.

Mwiko wake asile funo, mnyama mdogo wa porini jamii ya mbuzi na NYAKIHUKO, mnyama afananaye na panya. Pia asiokote kuni za mti uitwao MUNYATOMAA na kukokea moto. MUFWIMI alitoroka usiku kwa kuogopa kuuawa na Mwamududa ambaye kumbe alipopata taarifa za ujauzito wa binti yake, alifurahi sana kwa kujua kuwa sasa angeolewa kirahisi. MUFWIMI hakuwarudia tena wale wafuasi wake bali aliendelea kuwinda hadi huko ITAMBA, USUNGWA alikouawa na NYATI.

 

Wafuasi wake walipomtafuta, walipata taarifa za kuuawa kwake huko ITAMBA, lakini pia walipewa taarifa ambazo MUFWIMI aliwasimulia wakazi wa huko juu ya binti wa MWAMUDUDA aliyemwacha na ujauzito wake. 

Waliamua kwenda huko kwa kujifichaficha, lakini walipodhihirika, walikaribishwa vizuri na kupewa makazi na mtawala MWAMUDUDA aliyefurahi kupata mjukuu. Huyu MWAMUYINGA mtoto wa MUFWIMI, CHOTARA wa KIMANGA aliyekuwa jasiri tangu ujanani, alimrithi babu yake na kuanza kutawala sehemu hiyo ya NG’ULUHE akiwa ‘MUTWA’ wa kwanza wa kabila lililotoka nje ya Tanganyika. 

Ni kutokea kwa huyu MUYINGA wa kwanza ndipo ulifuatia mfululizo wa vizazi kupitia kwa watoto waliozaliwa, ambapo MALIGA alimzaa MUDEGELA aliyemzaa KILONGE aliyemzaa NGAWONA LUPEMBE aliyeuawa na mdogo wake MUNYIGUMBA, ambaye alianza kuitanua himaya ya Uhehe baada ya kushika utawala mnamo mwaka 1870.

Huyu aliwashinda kivita wababe wa KINITOLE na kuyaunganisha makabila ya Iringa, watu waliokuja kuitwa Wahehe na wakoloni hapo baadaye kutokana na mlio wao wa kivita wanapotupa mikuki kwa kusema he he he! wakiashiria hatari.

Kutoka Mutwa huyu ndipo alifuatia kutawala MUKWAVINYIKA, mtoto wa pili wa MUNYIGUMBA, ambaye jina lake mtawala huyu liliwashinda wakoloni kulitamka na hivyo kufupisha kwa kutamka MKWAWA. 

MKWAVINYIKA alianza kutawala akiwa na miaka 19 na aliyapiga vita makabila yote yaliyozunguka himaya yake na kuwashinda watu kama kina CHABULUMA, MTWA wa WANGONI na MERERE, shemeji wa MTWA wa WASANGU. MUKWAVINYIKA alipigana pia na wakoloni wa Kijerumani. 

Msomaji, simulizi hizi za Wahehe ni ndefu sana na zenye mambo mengi mno, ikiwemo kujipa majina ya kujitapa kulikofanywa kwa idhini ya Mutwa baada ya kutenda matendo makuu, ushujaa wa kutupa mikuki, uwezo wa mbio za kufukuza maadui, dawa za ushindi wa vita nakadhalika.
 

NAMNA YA KUHIFADHI KUMBUKUMBU ZA ASILI NA ZA KAUKI

CONSERVATION OF TRADITIONAL HERITAGE

Kuendelea kufundishwa kwa mada ya Historia na Chimbuko la Ukoo wa Kivenule, ni kichocheo kwa Wana-KAUKI kuendelea kutafiti taarifa mbalimbali zinazohusiana na Kabila lao la Wahehe. Ni fursa ya kuibua mijadala ambayo itasaidia kuleta njia mbadala za kuendelea kutunza kumbukumbu za asili na hususani mambo ya kale yanayohusiana na Kabila la Uhehe. Mila na Desturi za Kabila la Wahehe ambazo zinajumuisha Ustaarabu, Vyakula, Ngoma, Nyimbo, Mavazi na mambo mbalimbali yanayohusiana na Tunu za Mhehe zitaendelea kuenziwa endapo jamii yenye husika itaonesha nia dhabiti ya kutunza kumbukumbu hizi katika namna ambayo itakuwa na faida kwa kizazi kijacho.

Mada ya Historia na Chimbuko la Ukoo, huleta mjadala wa namna gani nzuri ya kuhifadhi kumbukumbu za ukoo; na pia njia bora za kuendelea kutunza taarifa zinazohusiana na Ukoo. Baadhi ya njia zilizopendekezwa ni pamoja na:

  • Kuchagua viongozi (uongozi) utakaokuwa na jukumu la kufuatilia taarifa mbalimbali zinazohusiana na ukoo na historia ya uhehe kwa ujumla katika maeneo mbalimbali; hususani katika maeneo ambayo wanadhani zinaweza kupatikana.
  • Pawepo na mfumo unaoeleweka wa kuhifadhi kumbukumbu aidha katika maandishi au namna nyingine yeyote.
  • Pawepo na taarifa za mara kwa mara katika maandishi ambazo zitakuwa zinawasilishwa wakati wa mikutano mikuu ya KAUKI.
  • Wajumbe wa mkutano walipendekeza umuhimu wa kumtumia Babu Hussein ambaye bado yupo hai kwa sababu ana taarifa nyingi zinazohu ukoo wa Kivenule.
  • Pia ilikubaliwa na wana-KAUKI kuwa licha ya kuwepo kwa majina ya kisasa na ya Ubatizo ambayo walipewa hawa Babu na Bibi zetu; ni vyema pia majina yote yakajumuishwa kwenye makaburi yao ikiwa ni sehemu mojawapo ya kutunza kumbukumbu. Majina mapya siyo maarufu (au hayafahamiki sana); kwa hiyo ni vyema bado tukaendelea kutumia majina yote ili tusipoteze kumbukumbu.
  • Yachongwe mawe yenye majina ya marehemu ambapo yatawekwa katika makaburi kwa sababu siyo rahisi kufutika na kupotea.
  • Taarifa za historia ya ukoo ni muhimu ziwekwe kwenye maandishi hususani vijitabu vidogo vidogo ambavyo vitasambwa kwa wanaukoo mbalimbali na kuweza kujisomea.
  • Mada hii ya Chimbuko na Historia ya Ukoo wa Kivenule, iwe ni mwendelezo wa taarifa mbalimbali ambazo tumekuwa tukizitafuta na kuziwasilisha katika Mikutano kama hii. Taarifa zinazopatikana katika mikutano mingine inayofanyika zisaidie kuziboresha taarifa za awali ambazo tayari zimepatikana na kuhifadhiwa. 

 

Tafsiri za Majina Mbalimbali yaliyopo katika Ukoo wa Kivenule

Kidagamhindi      Heka heka za kukimbia kodi wakati wa mkoloni

Tunyahindi          Kupigwa pigwa na wakoloni

Mwanitu              Alizaliwa kweusi (kwa kutumia lung’ali). Kuwasha moto ili
                          kupata mwanga kwa kutumia kuni au aina fulani ya nyasi.
                          Mara nyingi ving’ali vinakuwa vinazimika.

Kadungu              Kuwa na Dungu kubwa (kuwa na kitovu kikubwa)

Kibumo                Mvefi (Mtu anayelialia)

Mlagile                 Alizaliwa wakati Bibi yake hayupo. Wakati anaonyeshwa Bibi
                           yake akisema Mlagile  akaitwa Mlagile.

Fatamali               Alifuata mali

Yamkopita           Bibi alipomzaa mtoto wa kwanza na kisha kufariki, akapata
                          jina la ya Mkopite

Luhanage            Wakati Bibi anazaa watoto wanakufa, alipomzaa mtoto na
                          akaugua sana basi akaitwa Luhanage. Luhanage maana yake
                          ni kuugua sana.

Mgendwa            Alizaliwa kwa taabu. Alizaliwa kwa waganga wa kienyeji kwa
                         tabu wakiwa safarini

Msinziwa             

Kanolo                Wakati ameugua, anapiga ramli huki akitembea kwa waganga.

Yimilengeresa      Mzee Babu Husein alichukuliwa kwenye Vita ya Pili ya Dunia.
                          Wahindi walikufa sana na Waingereza wakashinda Vita.

 

Misamiti ya Lugha ya Kihehe

Mhisive                Binamu

Nyavana              Degedege

Ligalu                  Vita

Watavangu          Wakubwa (Wakuu wa Nchi) kabla ya Ukoloni

5 comments:

  1. NDUGU, hongera sana kwa kazi nzuri ambayo unaendelea kufanya. je una habari zozote kuhusu wahehe walowezi wa mufindi sehemu za ifwagi ilunda, nzivi na kihanga ya sasa? kuna koo za machifu kama mlekafike, kadendula, vangisada ambao ukoo wa akina miho unatokana nao? nawasilisha.

    ReplyDelete
  2. Hongereni sana, tuendelee kuiboresha hiyo historia kwa kuongezea maelezo muhimu, (historia ijitosheleze)

    ReplyDelete
  3. Safi sana...Huu ni mwanzo mzuri sana wa kujua tulikotoka, itasaidia sana kuona tunakokwenda

    ReplyDelete
  4. Hongera mno bila shaka nimepata maarifa kuhusu lughamama yangu

    ReplyDelete