Mchakato wa Kuandaa Kitabu cha Chimbuko, Muundo na Historia ya Ukoo wa Kivenule na Uhehe kwa Ujumla

Mchakato wa Kuandaa Kitabu cha Chimbuko, Muundo na Historia ya Ukoo wa Kivenule na Uhehe kwa Ujumla
Karibu uone yale ambayo KAUKI inafanya

Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI, 2014

Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI, 2014
Chimbuko na Muundo wa Ukoo wa Kivenule (2005 - 2009)

Mkutano Mkuu wa10 wa KAUKI

Mkutano Mkuu wa10 wa KAUKI
Tangazo la Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI

Wednesday 9 January 2013

RASLIMALI YA GESI MTWARA

MKANGANYIKO NAMNA YA KUNUFAIKA NA RASLIMALI WALIGUBIKA TAIFA

§   Wazawa zinakotoka Raslimali hizo wanufaike kwanza, kisha baadaye maeneo mengine 

Taifa limekumbwa na mgawanyiko mkubwa wa namna ya kunufaika na raslimali zinazopatikana hapa nchini. Uzoefu unaonesha kuwa, watanzania wengi bado hawajanufaika kikamilifu na raslimali za asili zinazopatikana kutoka katika maeneo yao. Maandamano yaliyofanywa na wananchi kutoka Mkoa wa Mtwara, ni mfano tosha kuonesha kilio chao cha muda mrefu cha kushindwa kunufaika na raslimali, hali ambayo wenye mamlaka na watunga sera inabidi wajifunze. 

Mkoa wa Mtwara, Lindi na Pwani imekuwa ni maarufu kwa kilimo cha Korosho, zao la biashara ambalo limechangia kwa kiwango kikubwa mapato ya kigeni. Korosho yenyewe haijawanufaisha kabisa wakazi wa mikoa hiyo na hususani Mtwara ambayo ilikuwa bado iko nyuma kielimu, kimiundombinu na kimaendeleo. Watunga sera na serikali kwa ujumla waliingilia kwa kiasi kikubwa kupitia Bodi ya Korosho kusimamia soko na uuzaji wa zao la Korosho. Matokeo ya udhibiti wa soko uliofanywa na serikali umeendelea kuwadidimiza wakulima hao na pia kudidimiza zao la biashara la Korosho na hivyo kuwasabishia machungu makubwa na umaskini. 

Waswahili wana msemo huu, "Uking'atwa na Nyoka, hata ukiguswa na ujani unashtuka". Wananchi wa Mtwara tayari wameng'atwa na nyoka kupitia zao la biashara la Korosho. Kwa sasa hawana imani tena na watunga sera na wasimamizi wa sera hizo. Wananchi hawa wana kilio cha kushindwa kunufaika na zao la Korosho na matokeo yake kuendelea kuwa masikini. 

Tofauti na ilivyotegemewa wengi, kuwa kwa sababu zao la Korosho bado lipo kwenye soko tofauti na zao la Kahawa na Pamba katika Mikoa ya Kilimanjaro, Kagera na Mwanza ambalo limekufa kabisa; ilibidi hali yao ya kiuchumi iwe juu.  Umasikini ni somo kwao. Wamelitambua tatizo walilonalo na pia wamejitambua. Ndiyo maana kwa sasa wameshikamana kuhusiana na mustakabali wa Gesi na Mafuta ambayo yamegundulika katika pwani ya Mnazi Bay, katika Mkoa wa Mtwara. 

Kwa nini wananchi hawa wanadai kuwa wa kwanza kunufaika na raslimali hii? Hii inatokana na mifano mbalimbali ambayo wanayo kutoka mikoa ya Shinyanga, Mwanza, Arusha, Kagera na Mara ambapo mikoa hii ilikuwa maarufu kwa uchimbaji wa Dhahabu, Almasi na Tanzanite. Je ni kwa kiwango gani mikoa hii imenufaika na raslimali hizo? 

Kwa upande wa Arusha huko Mererani Wilaya ya Simanjiro ambayo ni mtoaji wa Tanzanite pekee duniani, bado kabisa haijanufaika kikamilifu na raslimali hiyo. Wananchi wake bado ni maskini wa kupindukia. Madini ya Tanzanite yanapoteza umiliki wake halali kiasi cha nchi ya Kenya na Afrika Kusini kutawala soko la Tanzanite. Wananchi wa Mtwara wameyaona haya na ndiyo maana waliandamana kudai kunufaika na Gesi.  

Tanzanite imekuwa na mchango mdogo sana katika pato la Taifa licha ya kuwa ni madini pekee duniani yanayopatikana katika nchi ya Tanzania pekee. Hakuna usimamizi wa kina na mapato au bidhaa zinazotokana na raslimali hii. Mwekezaji mgodini hapo yaani Tanzanite One mkataba wake umeisha, lakini akapewa tena mkataba tata ambao wawakilishi wa wananchi wamepiga kelele sana huko bungeni lakini hawakusikilizwa. Wananchi wanaoishi kuzunguka katika migodi hii ni maskini wa kutupwa na wameangukia katika lindi la migogoro isiyoisha na hata wakati mwingine kupoteza maisha yao. Hili ni somo kwa wana Mtwara. 

Mikoa ya Shinyanga, Mwanza na Mara ilijaliwa kuwa na raslimali ya Dhahabu na Almasi. Matokeo ya kuwepo kwa raslimali hizo imesababisha mfarakano na vifo kwa wakazi wa mikoa hiyo. Kwa mfano katika Mgodi wa North Mara, wananchi wengi wamepoteza maisha kutokana na kuchafuliwa kwa mazingira na sumu, kuuawa na askari (kupigwa risasi) wakati wanapoenda kuokota mabaki ya mawe yaitwayo Magwangwala ambayo wanafikiria wakiyasaga wanaweza kupata kiasi kidogo cha madini ambayo wakiuza wanakidhi mahitaji yao; kuachiwa mashimo yasiyo na kitu, kupoteza mifugo kutokana na sumu; kuchafuliwa maji kutokana na kemikali zinazozagaa ovyo kwa sababu ya kushindwa kudhibiti uharibifu wa mazingara na pia kuangukia katika wimbi la umaskini. Wananchi hawa pia walizuiwa kushiriki katika uchimbaji mdogo mdogo wa madini ambao ungewasaidia kupata kipato na kuweza kupunguza umaskini, kusomesha watoto na pia kuzihudumia familia zao.  

Kama ilivyo kwa mgodi wa North Mara, huko Geita hali haikuwa tofauti  kwa sababu wananchi walihamishwa katika maeneo yao na kuachwa bila makazi. Baadhi ya vijana walifukiwa mashimoni katika maeneo ambayo walikuwa wanachimba dhahabu. Wachimbaji wadogo waliondolewa na kukosa kabisa eneo la kutafuta riziki yao. 

Kwa taarifa za sasa Ndugu Abrahman Kinana Katibu Mkuu wa CCM alitumia madaraka yake vibaya alipowapelekea wananchi wanaoishi karibu na mgodi wa GGM leseni tano za uchimbaji mdogo, badala ya shughuli hiyo kufanywa na wizara husika. Kitendo hiki kinatafsiriwa kuwa CCM inawajali wakaazi hao kuliko wizara husika yenye dhamana hiyo. 

 Hali kama hii pia iliukumba mgodi wa Bulyahulu ambapo kuna vijana wengi walifukiwa ndani ya migodi kwa kuelekezewa maji ya mvua. Uhamishwaji usiofuata taratibu na ukatili wa kila aina ulifanyika kwao. Matokeo yake wamebaki na wanaendelea kuwa masikini katika nchi yao yenye neema.  

Katika mkoa wa Kagera, Mwanza na Mara hali imendelea kuwa hivyo hivyo kama ilivyo mikoa mingine yenye raslimali. Kwa mfano wakazi wa mikoa inayozunguka Ziwa Victoria wameendelea kukosa kabisa haki ya kupata kitoweo cha samaki. Wameendelea kula mikia na vichwa maarufu kama mapanki huku minofu ikisafirishwa nje ya nchi. Bei ya samaki ni kubwa mno kiasi kwamba mwanachi maskini wa kawaida hawezi kumudu kumnunua samaki mmoja.  

Wananchi wa mikoa hiyo walikuwa na uvuvi wao wa asili huku wakilinda na kutunza mazingira ya ziwa hilo, lakini wawekezaji walikuja na jina lao, wanaitwa wavuvi haramu. Humo ziwani kuna aina nyingi ya samaki ambao wote waliliwa na Sangara aliyepandikizwa humo na kuua vizazi vya samaki asili wa ziwa hilo; lakini serikali inasimamia Sangara tu aina nyingine haitambuliwi kabisa. Ikumbukwe kuwa humo ziwani kuna aina ya samaki ambao hata wakiwa na miaka kumi hawakui kufikia inchi mbili. 

Hali kadhalika katika mgodi wa Almasi huko Shinyanga hali ya umaskini kwa wakazi wanaoendelea kuzunguka machimbo hayo ni kubwa na ya kutisha licha ya uchimbaji kuendelea kufanyika kwa takribani miaka 32. 

Wana Mtwara wasibezwe, waungwe mkono kwa sababu wamejitambua na huu ndiyo wajibu wao. Kisingizio cha kusema kuwa raslimali ziwanufaishe wananchi wote hii ni sawa lakini wenye nacho wapewe kipaumbele, kwa sababu hata maendeleo baina ya mikoa yametofautiana na hii ni sababu tosha.  

Pamekuwepo na kujipendelea kwa baadhi ya viongozi wanaopata fursa katika Baraza la Mawaziri kuelekeza uwingi wa raslimali katika mikoa, wilaya na kata zao. Mfano pekee ambao ninaoukumbuka ni kipindi ambapo Ndugu Basil Mrambo alipokuwa Waziri wa Fedha ambapoweza kutenga kiasi cha shilingi bilioni 9 katika barabara ya hadhi ya kata, kipindi hicho mikoa mingine ikishindwa kuunganishwa na barabara ya lami. Huu ni mfano mdogo lakini kuna mifano mingi.

Wana Mtwara pengine wameangalia asilimia ya fursa ambazo wamezipata wananchi kutoka katika mkoa huo katika vikao vya kufanya maamuzi pamoja na kutunga sera. Kunyimwa kwa fursa hizo za kufanya maamuzi pengine zimechangia kuifanya iendelee kuwa nyuma kimaendeleo.  

Uamuzi wa sasa wa kung'ang'ania kujenga bomba la gesi kuja Dar es Salaam kwa ajili ya kuzalisha umeme si la busara kabisa na ndiyo maana wakazi wa Mtwara wamelipinga. Kiasi cha Trilioni Moja kilichobajetiwa kujenga bomba, ni vyema kingetumika kununua mitambo ya kuzalisha umeme na kujengwa mkoani Mtwara. Hii itasaidia kuleta maendeleo katika mkoa wa Mtwara huku ikitoa changamoto ya kuwa na Kiwanda Kikubwa (Big Power Plant) ambazo itazalisha umeme ambao utaunganishwa kwenye gridi ya Taifa toka huko huko Mtwara. 

Pia siyo vyema na salama kila kitu kujengwa Dar es Salaam maana yanaweza kutokea maafa kama vita au mafuriko ya bahari ikizingatiwa kuwa Dar es Salaam ipo pembezoni mwa bahari. Ni vyema tukawa na maeneo mengi ambayo yana mitambo ya umeme tukaepuka nchi kuwa gizani kwa kuwa na chanzo kimoja kwenye umeme. Angalia hata viwanja vya ndege mbona vimejengwa maeneo mengi nchini siyo tu Dar, hii inasaidia kukuza uchumi wa nchi yetu. 

Mwisho wa maoni yangu. 

 

Imeandaliwa na:

Adam Kivenule

0713270364

kivenule@gmail.com

No comments:

Post a Comment